Kesha la asubuhi: WATENDAKAZI PAMOJA NA MUNGU

                 KESHA LA ASUBUHI
              ALHAMISI- JUNE 07, 2018
  WATENDAKAZI PAMOJA NA MUNGU
“Maana sisi tu wafanyakazi pamoja na Mungu; ninyi ni shamba la Mungu, ni jengo la Mungu.” (1 Wakorintho 3:9).

▶Lazima Roho Mtakatifu awe wakala hai wa kusadikisha juu ya dhambi. Wakala huyu wa kiungu humwasilishia mzungumzaji manufaa ya kafara iliyotolewa msalabani; na kadiri neno hili la kweli linapofikishwa kwa roho zilizopo, Kristo hujitwalia, na hutenda kazi ili kubadilisha tabia yao. Yuko tayari kusaidia udhaifu wetu, kutufundisha, kutuongoza, na kutuhamasisha kwa mawazo yenye asili ya mbinguni.

▶Ni kidogo jinsi gani wawezavyo kufanya wanadamu katika kazi ya kuokoa roho, na hata hivyo ni kubwa kiasi gani wanaweza kufanya kupitia Kristo, endapo wakijazwa Roho Wake! Mwalimu mwanadamu hawezi kusoma mioyo ya wasikilizaji wake; lakini Yesu hukirimu neema ambayo kila roho huhitaji. Yeye hufahamu vipaji vya mwanadamu, udhaifu na uimara wake. 

▶Bwana anatenda kazi ndani ya moyo wa mwanadamu; na mchungaji anaweza kuwa harufu ya mauti iletayo mauti kwa roho zinazoyasikiliza maneno yake, akiwageuzia mbali na Kristo; au, kama amejiweka wakfu, mcha-Mungu, asiyejitumainia nafsi, bali humwangalia Yesu, anaweza kuwa harufu ya uzima iletayo uzima kwa roho ambazo tayari ziko chini ya nguvu ya usadikisho wa Roho Mtakatifu, na ambao katika mioyo yao Bwana anaandaa njia kwa ajili ya ujumbe ambao amempatia wakala wa kibinadamu. Kwa namna hiyo moyo wa asiyeamini huguswa, naye huitikia na kuupokea ujumbe wa neno la kweli.

▶“Sisi tu wafanya kazi pamoja na Mungu.” Miguso ya usadikisho iliyopandikizwa moyoni, na kuelimishwa kwa ufahamu kupitia upokeaji wa Neno, hutenda kazi katika upatanifu kamili. Kweli iliyoletwa akilini ina uwezo wa kuamsha nguvu za roho zilizokufa. Roho wa Mungu atendaye kazi moyoni hushirikiana na utendaji wa Mungu kupitia mawakala Wake wa kibinadamu. 

▶Tena na tena nimeoneshwa kwamba watu wa Mungu katika siku hizi za mwisho wasingeweza kuwa salama kwa kuwatumainia wanadamu, na kuufanya mwili kuwa tegemeo lao. Shoka imara la neno la kweli limewachimbua kutoka ulimwenguni wakiwa kama mawe yakwaruzayo yanayopaswa kuchongwa na kunyooshwa na kulainishwa kwa ajili ya jengo la mbunguni. Wanapaswa kuchongwa na manabii kwa makaripio, maonyo, nasaha, na ushauri, ili waumbwe wafanane na Kielelezo cha kiungu; hii ndiyo kazi maalumu ya Mfariji—kubadilisha moyo na tabia, ili wanadamu waifuate njia ya Bwana.

Leave a Reply