Kesha la asubuhi: NURU YA ULIMWENGU

                   KESHA LA ASUBUHI

                 JUMAMOSI   02/05/2018

              *NURU YA ULIMWENGU? _“Ninyi ni nuru ya ulimwengu. Mji hauwezi kusitirika ukiwa juu ya mlima” Mathayo 5:14_

✍?Uaminifu wetu kwa kanuni za Ukristo unatuita kwa huduma ya utendaji kwa ajili ya Mungu. Wale ambao hawatumii talanta zao katika kazi na kusudi la Mungu hawatakuwa na sehemu pamoja na Kristo katika utukufu wake. Nuru haina budi kuangaza kutoka katika kila roho iliyopokea neema ya Mungu. Roho nyingi zimo gizani, lakini wengi wanajisikia pumziko, raha na utulivu katika hali hiyo! 

✍?Maelfu wanafurahia nuru kubwa na fursa za thamani, lakini hawafanyi cho chote kwa mvuto wao au fedha yao, ili kuwaangazia wengine nuru. Hawachukui hata jukumu la kutunza roho zao wenyewe katika upendo wa Mungu, ili kwamba wasiwe mzigo kwa kanisa. 

✍?Watu wa jinsi hiyo watakuwa ni mzigo na kizuizi mbinguni. Kwa ajili ya Kristo, kwa ajili ya ile kweli, na kwa ajili yao wenyewe, wanapaswa kuamka na kufanya kazi kwa bidii kwa ajili ya umilele. Makao ya mbinguni yanaandaliwa kwa ajili ya wale ambao watakubaliana na masharti yaliyowekwa wazi katika Neno la Mungu.

✍?Kwa niaba ya roho zile ambazo Kristo alizifia, wale ambao wamo katika giza la makosa, wafuasi wote waaminifu wa Kristo wameamriwa kuwa nuru kwa ulimwengu. Mungu amefanya sehemu yake katika kazi hii kuu, na anangojea ushiriki wa wafuasi wake.

✍? Mpango wa wokovu umekamilika kabisa. Damu ya Yesu Kristo imetolewa kwa ajili ya dhambi za ulimwengu, Neno la Mungu linazungumza na binadamu katika mashauri, makaripio, maonyo, ahadi, na kutia moyo, na ufanisi wa Roho Mtakatifu unatolewa ili kumsaidia katika juhudi zake zote. Lakini pamoja na nuru yote hiyo ulimwengu bado unaangamia gizani, ukiwa umezama katika makosa na dhambi.

??‍♂```Ni nani watakaokuwa watendakazi pamoja na Mungu, ili kuleta hizi roho katika kweli? Ni nani atakayewapelekea habari njema za wokovu? Watu ambao Mungu amewabariki kwa nuru na kweli wanapaswa kuwa wajumbe wa rehema.Utajiri wao unapaswa kutiririka kupitia katika mfereji wa kimbingu. 

??‍♂Juhudi zao za dhati hazina budi kuonekana. Imewapasa kuwa watendakazi pamoja na Mungu, wenye kujikana nafsi, wenye kujitolea, sawa na Yesu, ambaye kwa ajili yetu alikuwa maskini, ili kwamba kupitia umaskini wake, sisi tupate kuwa matajiri. – Review and Herald, Machi 1, 1887.```

*MUNGU AKUBARIKI MUWE NA SIKU NJEMA*

Leave a Reply